Jumatatu, 6 Mei 2013

SKAUTI MKUU MTEULE ASABAHIANA NA SKAUTI

Skauti Mkuu Mh. Mwantum Mahiza akivalishwa Skafu na Skauti mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa Don Bosco Upanga jijini Dar Es Salaam kuwasabahi Skauti tarehe 06/05/2013
Mh. Mwantum Mahiza akisaini kitabu cha wageni
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mh. Mwantum Mahiza ambaye ni Skauti Mkuu Mteule aliwasabahi Skauti wa Mkoa wa Dar Es Salaam katika ukumbi wa Don Bosco Upanga jijini Dar Es Salaam kabla ya kikao na kamati ya mpito, kamati tendaji na wakufunzi wa Skauti Makao Makuu ya Skauti, Mh. Mahiza aliteuliwa na Mlezi wa Skauti Tanzania Mh. Dkt Jakaya Kikwete (Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania) tarehe 19 Aprili, 2013. Mh. Mwantum pia alisaini kitabu ikiwa kama ishara yake ya kufika ofisini Makao Makuu ya Skauti kuanza kazi. 
Mh. Mahiza alitoa shukrani zake kwa Skauti wa Tanzania kwa demokrasia waliyoitumia baada ya uchaguzi katika Mkutano Mkuu Maalum wa Baraza Kuu uliofanyia tarehe 05 Januari, 2013 na hatimaye tarehe 19 Aprili, 2013 kuteuliwa kuwa Skauti Mkuu Tanzania.

Katika salamu zake Mh. Mahiza aliwasisitiza Skauti Tanzania kuwa na mshikamano, uadilifu, imani, na kuwakumbusha Skauti kuwa yaliyopita si ndwele. "Binadamu si wakamilifu tusichukulie udhaifu wetu kuharibu Skauti Tanzania" alisema Mh. Mahiza. Aliongeza kusema "Nina maanisha kweli kweli Skauti wana imani na mimi, nami si malaika lakini nina imani kubwa ya kuleta mabadiliko ambayo yataleta hofu, kubwa zaidi bila ya ushirikiano wenu basi hatutafika" 

Aliwataka Skauti kuweka chama mbele na mtu nyuma ili katika kurudisha imani ya Skauti kwa jamii.
Mh. Mwantum Mahiza Skauti Mkuu Mteule akionyesha Kiruhusishi (Warrant) chake cha Uteuzi wa Skauti Mkuu kwa Skauti waliohudhuria katika mazungumzo, wa kwanza kushoto aliyesimama ni Mwenyekiti wa kamati ya mpito Brigedia Jenerali Mstaafu Gerald Mkude, katika Ukumbi wa Don Bosco Upanga Dar Es Salaam tarehe 06 Mei, 2013.

MKUTANO MKUBWA 

Mh. Mahiza alisisitiza kuwa ana tabia ya kusamehe kabla ya kuomba msamaha, pia aliwataka Skauti Tanzania kusameana kwanza na kufungua ukurasa mpya.
"Miezi miwili baada ya kuapishwa kwangu, tutakuwa na mkutano mkubwa ambao tutautumia katika kuleta mabadiliko na mafanikio zaidi, pamoja na kuipitia katiba yetu, muundo wa Skauti je, upo sawa, viongozi tuliopo tunafaa? ndiyo au hapana?" alisema Skauti Mkuu Mteule.

Mh. Mahiza alisema pia, mabadiliko yanaweza kuwafurahisha na kuwachukiza wengine lakini aliwakumbusha Skauti kukumbuka na kuzingatia kiapo cha chama.

MAKUNDI

Mh. Mahiza aliyesimama akisisitiza jambo.
Skauti Mkuu Mteule Mh. Mahiza aliwakumbusha Skauti kuwa makundi hayana maendeleo yeyote na kuwataka Skauti kuwa na kaliba na weledi nzuri ili kukijenga chama, aliwataka Skauti Tanzania wajue kuwa amekuja kuimarisha chama na kuwataka Skauti wasameheane saba mara sabini kwani hakuna mtu aliye msafi, Skauti ni mapenzi ya mtu kwahiyo ushirikiano ni muhimu sana kwani kuna majanga mengi na Skauti tuwe wepesi katika matatizo ya kijamii na mfano wa kuigwa kwa jamii. Katika kusaidia watoto, kuzuia uhalifu na kufundisha stadi na maalifa ya Skauti mashuleni.
Mh. Mahiza alikemea makundi kwani makundi utoa imani na kuleta jambo kubwa baya, "Tunahitaji kufanya mabadiliko yatakayo fufua Skauti kwa kufanya mema, mabadiliko kwa kushirikiana sote tuelezane mabaya na mema" alisema Mh. Mahiza.

Skauti Mkuu alitahadharisha kuwa katika Skauti hakuna Siasa, Udini wala Ukabila na hatokubali hayo katika uongozi wake.

Kiruhusishi (Warrant) ya Skauti Mkuu Mteule Mh. Mahiza

Barua ya kuteuliwa kuwa Skauti Mkuu kwa Mh. Mahiza
Baadhi ya Skauti walioudhulia maongezi na Skauti Mkuu Mteule katika ukumbi wa Don Bosco Upanga, Dar Es Salaam.