Jumamosi, 8 Juni 2013

SKAUTI WA DAR-ES-SALAAM WAFANYA ZIARA YA UTALII WA NDANI

  • Waenda Mbuga ya Mikumi na Kambi ya Bahati Morogoro

Baadhi ya Skauti wakiwa katika kiwanja cha Makao Makuu ya Skauti Upanga, Dar Es Salaam.

Skauti wa Wilaya ya Temeke, Ilala na Kinondoni kutoka Mkoa wa Dar Es Salaam wanafanya ziara ya Kimafunzo na Utalii wa ndani mkoani Morogoro, ziara hiyo itakuwa ya siku tatu kuanzia tarehe 08 Juni, 2013. Kwa mujibu wa kiongozi wamsafara huo Skauta Heldon Mwaipopo alisema, "Ziara hii ni ya kielimu, utalii na mafunzo kwa skauti vijana wa shule ya msingi kwa lengo la kuwafundisha vijana kwa ualisia mambo mbalimbali ya kitalii katika nchi yetu" Pamoja na hayo Skauti hao watapata fursa nzuri ya kutembelea mbuga ya wanyama ya Mikumi na Milima ya Uruguru mkoani Morogoro. Ndugu Mwaipopo aliendelea kusema "Pia vijana wetu watapata nafasi ya kuona wanayojifunza katika masomo yao na vilevile katika mafunzo ya Skauti ambayo yatawasaidia kiafya na kuwajengea uwezo wao wa kufikiri na kutenda vyema katika masomo yao ya darasani na maisha yao ya kila siku"
Heldon Mwaipopo Kiongozi wa ziara
Skauti 158 wameshiriki katika ziara hiyo ya kielimu na utalii wa ndani.
Pamoja na hayo yote ndugu Mwaipopo aliendelea kusema "Tunashukuru kwa ushirikiano wa walimu, wazazi na walezi kwa kuwakubalia watoto wao katika ziara hii, kuwepo kwa pamoja vijana hawa 158 kutoka katika maeneo tofauti na rika tofauti kiujumla watapata changamoto ya kujadiliana na kubadilishana mawazo jinsi wanavyoishi, na huu ni mpango endelevu tunawakaribisha zaidi vijana na baada ya siku tatu tutakuwa na ziara nyingine tena"

Moja ya basi walilosafiria Skauti kwenda Morogoro
Katika ziara hiyo ambayo ilikuwa na mabasi madogo aina ya Toyota Coaster sita, skauti watapata nafasi ya kutembelea kambi ya kitaifa ya Bahati (Bahati Camp), Mbuga ya wanyama ya Mikumi na Milima ya Uruguru kuanzia tarehe 08 mpaka 11 Juni 2013. Mwalimu Mwinuka kutoka shule ya msingi ya Kisukulu alisema "Ziara hii tumeiandaa rasmi kwa ajili ya utalii wa ndani ambayo itawasaidia watoto kubadilisha mazingira na hasa kimasomo kuangalia mbuga na wanyama na kujifunza aina mbalimbali ya wanyama, ndege na pia kuangalia milima na uoto wa asili wa sehemu furani na nyingine tofauti yake nini itasaidia watoto kuelewa masomo yao na pale linapokuja swali la mazingira, ndege na wanyama watakuwa tayari wameona na kuelezewa hali halisi. Na sisi kama Skauti tutakuwa tayari kuelezea jamii kuhusu utalii wa ndani na kuwafanya wageni kutembelea kwani nasi tumevutiwa sana"
Baadhi ya wanafunzi wanaoshiriki mafunzo hayo walielezea furaha yao ya kupata nafasi hii. Mtoto Salim Hassani na Selemani Sudi toka shule ya Msingi Rutihinda walionyesha furaha yao juu ya safari hiyo ambayo kwa upande wa shule hiyo waliongozwa na Mwalimu Kilindo Johnson.
Kamishna Peter Paul
Kamishna wa Skauti Mkoa wa Dar Es Salaam alisema "Safari hii ni Mafunzo ya Skauti, kimsingi ni sehemu moja ya mipango ya Skauti ambazo lazima zifanywe ili kuonyesha kuwa Skauti hipo na hii ni sehemu mojawapo ya mipango ya makundi" 
Katika hatua nyingine Kamishna Msaidizi wa Skauti Wilaya ya Ilala anafuatilia kwa karibu ziara hii katika hatua ya kuakikisha kuwa ratiba na mipango hiyo inafuatwa kama ilivyopangwa, zaidi Kamishna Peter Paul alisema "Mimi nitaondoka na usafiri tofauti katika kufuatilia nidhamu ya Skauti inafuatwa kwa mujibu wa ahadi na kanuni zetu"