Ijumaa, 24 Machi 2017

TSA yawawezesha Waelekezaji wa 'U-Report'

Balo Emmanuel, Meneja wa Mradi wa U-Report kutoka UNICEF akielezea jambo katika Warsha ya Wawezeshaji wa mradi huo katika Ukumbi wa hotel ya Ndekha jijini Dar es Salaam, tarehe 23/03/2017 (Picha na Sassi)


Habari na Crispin Majiya (PR Lab), Dar es Salaam


Chama cha Skauti Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa kuhudumia Watoto (UNICEF) kimefanya Warsha ya Siku Mbili Jijini Dar es Salaam yenye lengo la kuwawezesha Makamishna wa Mikoa na Wilaya pamoja na Wawakilishi wa Majukwaa ya Vijana kutoka Mikoa na Wilaya zao.

Warsha hii ni Awamu ya kwanza ya Mradi wa U-Report unaotekelezwa na Chama cha Skauti Tanzania, chini ya Udhamini wa UNICEF, ambapo katika Awamu hii Washiriki wanawezeshwa kuwa Waelekezi ambao watarudi Mikoani kwao kufundisha Vijana ambapo kila Kamishna wa Mkoa atawezeshwa kufanya kambi yenye Washiriki Vijana wasiopungua Sitini. hii itakuwa ni Awamu ya Pili ya Mradi wa U-Report.
Bi. Easter Peter Riwa Mkurugenzi Msaidizi Kazi na Maendeleo ya Vijana na Watu Walemavu Ofisi ya Waziri Mkuu akifungua Warsha hiyo.
U-Report ni programu maalum kwa ajili ya kutoa taarifa kwa matukio mbalimbali yanayotokea kwenye jamii zetu kama vile unyanyasaji wa watoto / kijinsia, matukio ya uhalifu, ajira za utotoni na ukatili dhidi ya watoto.

Aidha, imetolewa rai ya kujiunga kwa kutumia sms yenye neno 'SAJILI' kwenda namba '15070' na sms zote ni Bure (bila ya kutozwa gharama yoyote).

Huduma hii inapatikana kwa watumiaji wa mitandao ya simu ya kiganjani ya Tigo, Vodacom, Airtel na Zantel. Aidha mradi huo unatarajia kujiunga na mitandao mingine ya simu ya kiganjani ya Halotel pamoja na TTCL.

Aidha pamoja na uwezeshaji huu, washiriki walipata mafunzo kuhusu baadhi ya Sera za Chama cha skauti Tanzania jinsi zinavyoendana na programu hii ya U-Report. Sera hizo ni Sera ya Ulinzi wa Mtoto, Sera ya Programu za Vijana pamoja na Programu yenyewe. Pia walijifunza kuhusu Jinsi U-Report inavyoweza kutumika katika Ujumbe wa Amani (MoP) na Majadiliano, na kukabiliana na Maafa.



Baadhi ya washiriki wa Warsha wakisikiliza kwa makini



Mhariri na Picha: Sassi
Habari kwa Msaada wa TSA-PR Lab
(c)Tanzania Scouts Association - PR Lab 2017